Social Icons

Tuesday, July 12, 2011

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Serikali imehuzunishwa sana na tukio la jana wakati wa mchezo wa fainali ya Kombe la Kagame kati ya vilabu vya Simba na Yanga ambapo umeme ulikatika ghafla kwenye Uwanja wa Taifa. Wizara inawaomba radhi wapenzi wa soka wa Tanzania na Afrika Mashariki na Kati kwa usumbufu uliojitokeza.

Tukio hilo ambalo siyo la kawaida halikutazamiwa. Tunapenda kuwaahidi wananchi, hususani wapenda michezo, kwamba tukio la aina hiyo halitatokea tena. Aidha, Serikali inawashukuru wananchi wote waliojitokeza uwanjani hapo kushuhudia mchezo wa jana kwa kuwa watulivu wakati wote wa tukio hilo hadi umeme uliporejeshwa.

Kwa kutambua uzito wa suala hili, Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo imeunda Kamati ya watu wanne (4) kuchunguza sababu zilizosababisha umeme kukatika na kukosekana uwanjani hapo. Kamati hiyo itaongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara, Bi. Sihaba Nkinga. Wajumbe wengine ni Bw. Charles Bagenda, Mkuu wa Kitengo cha Umeme cha Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Bw. Mohamed Kiganja, Kaimu Katibu Mkuu, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Bi. Anna Chungu, Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi na Ugavi Wizarani.

Kamati itakamilisha kazi yake ndani ya siku saba (7) kuanzia kesho tarehe 12 Julai, 2011 na itakabidhi taarifa yake kwa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dkt. Emmanuel J. Nchimbi (Mb).

Wizara inapenda kutumia fursa hii kuzipongeza timu za Simba, Yanga na Ocean View zilizoshiriki kwenye mashindano ya mwaka huu kwa kuonyesha kiwango kizuri cha mchezo na nidhamu ya hali ya juu. Aidha, Wizara inaipongeza klabu ya Yanga kwa kuibuka mshindi.



Imetolewa na:-

KATIBU MKUU,

WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO

Tarehe: 11 Julai, 2011

No comments:

Post a Comment

Thank you for your comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...